Ninaitwa Agostino na nina umri wa miaka 51. Kazi yangu ni kusambaza chakula kwa baiskeli. Nina mabinti wawili, lakini ninaongea nao mara chache sana. Mimi na mama yao hatuishi pamoja tena kwa sababu tumeachana.
Miezi michache iliyopita, nilikuwa nikifanya kazi kama bawabu katika kampuni. Nilitengeneza vitu vilivyoharibika, nilibeba maboksi, na nilimsaidia yeyote aliyehitaji msaada. Siku moja, kampuni ilinifukuza kazi. Sikujua ni kwa nini.
Niliwaona watu wengi wakileta chakula kwa baiskeli. Ninaweza kuendesha baiskeli, kwa hiyo niligonga mlango wa kampuni kubwa ya usambazaji. Walinipa yuro tatu kwa kila safari. Ninaingiza yuro 40 kwa siku, yuro 60 nikibahatika sana, na wateja wananiongezea.
Sipati likizo ya malipo, hakuna malipo ya kuugua, na haki mbalimbali kwa ujumla. Sidhani kama hii ni sawa, lakini ninahitaji kazi. Waajiriwa wengi ni wahamiaji kutoka sehemu mbalimbali duniani.
Watu wengi wanaofanya kazi ya usambazaji wanaumia katika ajali kila siku. Baadaye, wakati kijana wa miaka 25 anayefanya kazi hii alipogongwa na gari na akafa, mamlaka zikaanza kututambua. Ni aibu kwa sababu hili lilitokea baada ya yeye kufariki.
Kwa kushirikiana na madereva wengine wa usambazaji kutoka katika makampuni mengine, nilisoma kozi inayohusu haki za wafanyakazi katika chama fulani nchini. Walitupa ushauri wa kisheria bure kabisa. Tukapambana ili tutambulike na tupate haki zaidi.
Baada ya muda mrefu, jitihada zetu zikazaa matunda. Kampuni moja kubwa ya usambazaji ililazimika kulipa faini kubwa na kuwapa wafanyakazi wake ajira za kudumu. Ilikuwa ni mara ya kwanza jambo kama hili kutokea duniani. Inaonekana kama mambo yameshaanza kuboreshwa.